___Translations___

_Quran?_

_Gadgets_

_Search_

_Links_

_Contribute_

_Note_

1 - AL-FAATIH'A
2 - AL - BAQARA
3 - AL I'MRAN
4 - AN-NISAAI
5 - AL - MAIDA
6 - AL - AN-A'AM
7 - AL - A'RAAF
8 - AL - ANFAAL
9 - AT-TAWBA
10 - YUNUS
11 - HUD
12 - YUSUF
13 - AR-RAA'D
14 - IBRAHIM
15 - AL - HIJR
16 - AN NAH'L
17 - AL ISRAAI (BANI ISRAIL)
18 - AL - KAHF
19 - MARYAM
20 - T'AHA
21 - AL - ANBIYAA
22 - AL -HAJJ
23 - AL - MUUMINUN
24 - AN - NUR
25 - AL - FURQAN
26 - ASH-SHUA'RAA
27 - AN-NAML
28 - AL-QAS'AS'
29 - AL - A'NKABUT
30 - AR-RUM
31 - LUQMAN
32 - ASSAJDAH
33 - AL-AH'ZAB
34 - SABAA
35 - FAAT'IR
36 - YA-SIN
37 - ASS'AFFAT
38 - S'AAD
39 - AZZUMAR
40 - GHAAFIR (AU AL MUUMIN)
41 - FUSS'ILAT (AU H'A MIM SAJDAH)
42 - ASH-SHUURA
43 - AZZUKHRUF
44 - ADDUKHAN
45 - AL - JAATHIYA
46 - AL - AH'QAAF
47 - MUH'AMMAD
48 - AL FAT-H'I
49 - AL H'UJURAAT
50 - QAAF
51 - ADH-DHAARIYAAT
52 - ATT'UR
53 - ANNAJM
54 - AL-QAMAR
55 - ARRAH'MAN
56 - AL -WAAQIA'H
57 - AL -H'ADIID
58 - AL - MUJAADALAH
59 - AL - H'ASHRI
60 - AL - MUMTAH'INAH
61 - ASS'AF
62 - AL - JUMUA'
63 - AL - MUNAAFIQUN
64 - ATTAGHAABUN
65 - ATT'ALAAQ
66 - ATTAH'RIIM
67 - AL - MULK
68 - AL - QALAM
69 - AL - H'AAQQAH
70 - AL - MAA'RIJ
71 - NUH'
72 - AL - JINN
73 - AL - MUZZAMMIL
74 - AL - MUDDATHTHIR
75 - AL - QIYAMAH
76 - AL - INSAN
77 - AL - MURSALAAT
78 - ANNABAA
79 - ANNAZIA'AT
80 - A'BASA
81 - ATTAKWIR
82 - AL - INFIT'AAR
83 - AL - MUT'AFFIFIIN
84 - AL - INSHIQAAQ
85 - AL - BURUUJ
86 - ATT'AARIQ
87 - AL - AA'LAA
88 - AL - GHAASHIYAH
89 - AL - FAJR
90 - AL - BALAD
91 - ASH-SHAMS
92 - AL - LAYL
93 - WADH-DHUH'AA
94 - ASH-SHARH'
95 - AT-TIN
96 - AL - A'LAQ
97 - AL - QADR
98 - AL - BAYYINAH
99 - AZ-ZILZALAH
100 - AL - A'ADIYAAT
101 - AL - QAARIA'H
102 - AT-TAKAATHUR
103 - AL - A'S'R
104 - AL - HUMAZAH
105 - AL - FIIL
106 - QURAISH
107 - AL - MAAU'N
108 - AL - KAWTHAR
109 - AL - KAFIRUN
110 - ANNAS'R
111 - AL - MASAD
112 - AL - IKHLAS'
113 - AL - FALAQ
114 - ANNAS
KISWAHILI

8 - AL - ANFAAL

 

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU.

 
1Wanakuuliza juu ya Ngawira. Sema: Ngawira ni ya Mwenyezi Mungu na Mtume. Basi mcheni Mwenyezi Mungu na suluhisheni mambo baina yenu, na mt'iini Mwenyezi Mungu na Mtume wake ikiwa nyinyi ni Waumini.
 
2Hakika Waumini ni wale ambao anapo tajwa Mwenyezi Mungu nyoyo zao hujaa khofu, na wanapo somewa Aya zake huwazidisha Imani, na wakamtegemea Mola wao Mlezi.
 
3Hao ambao wanashika Sala na wanatoa katika yale tunayo waruzuku.
 
4Hao kweli ndio Waumini. Wao wana vyeo, na maghfira, na riziki bora, kwa Mola wao Mlezi.
 
5Kama Mola wako Mlezi alivyo kutoa nyumbani kwako kwa Haki, na hakika kundi moja la Waumini linachukia.
 
6Wanajadiliana nawe kwa jambo la Haki baada ya kwisha bainika, kama kwamba wanasukumwa kwenye mauti nao wanaona.
 
7Na Mwenyezi Mungu alipo kuahidini kuwa moja katika makundi mawili ni lenu. Nanyi mkapenda lisilo na nguvu ndio liwe lenu; na Mwenyezi Mungu anapenda ahakikishe Haki kwa maneno yake, na aikate mizizi ya makafiri.
 
8Ili ahakikishe Haki na auvunje upotovu na wangachukia wakosefu.
 
9Mlipo kuwa mkimuomba msaada Mola wenu Mlezi, naye akakujibuni kuwa: Kwa yakini Mimi nitakusaidieni kwa Malaika elfu wanao fuatana mfululizo.
 
10Na Mwenyezi Mungu hakufanya haya ila kuwa ni bishara na ili nyoyo zenu zituwe. Na haupatikani ushindi ila kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye nguvu, na Mwenye hikima.
 
11Alipo kufunikeni kwa usingizi uwe ni uaminisho kutoka kwake, na akakuteremshieni maji kutoka mbinguni ili kukusafisheni kwayo na kukuondoleeni uchafu wa Shet'ani, na kuzipa nguvu nyoyo zenu, na kuitia imara miguu yenu.
 
12Mola wako Mlezi alipo wafunulia Malaika: Hakika Mimi ni pamoja nanyi, basi watieni nguvu walio amini. Nitatia woga katika nyoyo za walio kufuru. Basi wapigeni juu ya shingo na wapigeni kwenye kila ncha za vidole.
 
13Hayo ni kwa sababu wamemuasi Mwenyezi Mungu na Mtume wake. Na mwenye kumuasi Mwenyezi Mungu na Mtume wake basi Mwenyezi Mungu ni Mkali wa kuadhibu.
 
14Ndio hivyo! Basi ionjeni! Na bila ya shaka makafiri wana adhabu ya Moto.
 
15Enyi Mlio amini! Mkikutana na walio kufuru vitani msiwageuzie mgongo.
 
16Na atakaye wageuzia mgongo wake siku hiyo - isipo kuwa kwa mbinu za vita au kuungana na kikosi - basi atakuwa amestahiki ghadhabu ya Mwenyezi Mungu. Na pahala pake ni Jahannamu, na huo ni mwisho muovu.
 
17Hamkuwauwa nyinyi lakini Mwenyezi Mungu ndiye aliye wauwa. Na wewe hukutupa, walakini Mwenyezi Mungu ndiye aliye tupa, ili awajaribu Waumini majaribio mema yatokayo kwake. Hakika Mwenyezi Mungu ndiye Msikizi na Mjuzi.
 
18Ndio hivyo! Na hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye kudhoofisha vitimbi vya makafiri.
 
19Kama mnataka hukumu basi hukumu imekwisha kujieni. Na mkiacha itakuwa ndio kheri kwenu. Na mkirejea Sisi pia tutarejea. Na jeshi lenu halitakufaeni kitu, japo likiwa kubwa. Kwani hakika Mwenyezi yu pamoja na Waumini.
 
20Enyi mlio amini! Mt'iini Mwenyezi Mungu na Mtume wake, wala msijiepushe naye, nanyi mnasikia.
 
21Wala msiwe kama wale wanao sema: Tumesikia, na kumbe hawasikii.
 
22Hakika vinyama viovu mbele ya Mwenyezi Mungu ni vile viziwi na bubu visio tumia akili zao.
 
23Na Mwenyezi Mungu angeli jua wema wowote kwao ange wasikilizisha, na lau ange wasikilizisha wangeli geuka wakapuuza.
 
24Enyi mlio amini! Muitikieni Mwenyezi Mungu na Mtume anapo kuitieni jambo la kukupeni uzima wa milele. Na jueni kuwa Mwenyezi Mungu huingia kati ya mtu na moyo wake, na kwamba hakika kwake Yeye tu mtakusanywa.
 
25Na jikingeni na Fitna ambayo haitowasibu walio dhulumu peke yao kati yenu. Na jueni kuwa Mwenyezi Mungu ni Mkali wa kuadhibu.
 
26Na kumbukeni mlipo kuwa wachache, mkionekana wanyonge katika nchi, mnaogopa watu wasikunyakueni, naye akakupeni pahala pazuri pa kukaa, na akakutieni nguvu kwa nusura yake, na akakupeni riziki nzuri ili mpate kushukuru.
 
27Enyi mlio amini! Msimfanyie khiana Mwenyezi Mungu na Mtume, wala msikhini amana zenu, nanyi mnajua.
 
28Na jueni ya kwamba mali zenu na wana wenu ni Fitna (mtihani), na kwamba kwa Mwenyezi Mungu upo ujira mkubwa.
 
29Enyi mlio amini! Mkimcha Mwenyezi Mungu atakupeni kipambanuo, na atakufutieni makosa, na atakusameheni, na Mwenyezi Mungu ni Mwenye fadhila kubwa.
 
30Na walipo kupangia mpango walio kufuru wakufunge, au wakuuwe, au wakutoe. Wakapanga mipango yao, na Mwenyezi Mungu akapanga yake. Na Mwenyezi Mungu ndiye mbora wa mipango.
 
31Na wanapo somewa Aya zetu, wao husema: Tumesikia. Na lau tungeli penda tunge sema kama haya. Haya si chochote ila hadithi za watu wa kale tu.
 
32Na walipo sema: Ee Mwenyezi Mungu! Ikiwa haya ni kweli itokayo kwako basi tunyeshee mawe kutoka mbinguni, au tuletee adhabu yoyote iliyo chungu.
 
33Na Mwenyezi Mungu hakuwa wa kuwaadhibu nawe umo pamoja nao, wala Mwenyezi Mungu si wa kuwaadhibu na hali ya kuwa wanaomba msamaha.
 
34Lakini wana jambo gani hata Mwenyezi Mungu asiwaadhibu, na hali ya kuwa wanawazuilia watu Msikiti Mtakatifu? Wala wao hawakuwa ndio walinzi wake, bali walinzi wake hawakuwa ila wacha-Mngu tu. Lakini wengi katika wao hawajui.
 
35Na haikuwa ibada yao kwenye hiyo Nyumba (Al Kaaba) ila ni kupiga miunzi na makofi. Basi onjeni adhabu kwa vile mlivyo kuwa mkikufuru.
 
36Hakika wale walio kufuru hutoa mali yao ili kuzuilia Njia ya Mwenyezi Mungu. Basi watayatoa, kisha yatakuwa juu yao majuto, na kisha watashindwa. Na wale walio kufuru watakusanywa kwenye Jahannam.
 
37Ili Mwenyezi Mungu apate kuwa pambanua walio waovu na walio wema, na kuwaweka waovu juu ya waovu wengine, na kuwarundika wote pamoja, na kuwatupa katika Jahannam. Hao ndio walio khasirika.
 
38Waambie wale walio kufuru: Wakikoma watasamehewa yaliyo kwisha pita. Na wakiyarudia basi imekwisha pita mifano ya wa zamani.
 
39Na piganeni nao mpaka isiwepo fitna na mateso, na Dini yote iwe kwa ajili ya Mwenyezi Mungu. Lakini wakiacha, basi hakika Mwenyezi Mungu anayaona wanayo yatenda.
 
40Na kama wakigeuka basi jueni kwamba Mwenyezi Mungu ndiye Mola wenu, ni Mola Mwema na Msaidizi Mwema.
 
41NA JUENI ya kwamba ngawira mnayo ipata, basi khums (sehemu moja katika tano) ni kwa ajili ya Mwenyezi Mungu na Mtume, na jamaa, na mayatima, na masikini, na wasafiri, ikiwa nyinyi mmemuamini Mwenyezi Mungu na tuliyo yateremsha kwa mja wetu siku ya kipambanuo, siku yalipo kutana majeshi mawili. Na Mwenyezi Mungu ni Muweza wa kila kitu.
 
42Kumbukeni pale mlipo kuwa nyinyi kwenye ng'ambo ya karibu ya bonde, na wao wakawa ng'ambo ya mbali, na msafara ulipo kuwa chini yenu. Na ingeli kuwa mmeagana mngeli khitalifiana katika miadi. Lakini (mkakutana) ili Mwenyezi Mungu atimize jambo lilio kuwa lazima litendeke, kwa sababu aangamie wa kuangamia kwa dalili zilizo dhaahiri, na asalimike wa kusalimika kwa dalili zilizo dhaahiri. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusikia Mwenye kujua.
 
43Kumbuka alipo kuonyesha usingizini mwako kwamba wao ni wachache - na lau angeli kuonyesha kuwa ni wengi, mngeli ingiwa na woga, na mngeli zozana katika jambo hilo. Lakini Mwenyezi Mungu kakuvueni. Hakika Yeye ni Mwenye kuyajua yalio vifuani.
 
44Na mlipo kutana akakuonyesheni machoni mwenu kuwa wao ni wachache, na akakufanyeni nyinyi ni wachache machoni mwao, ili Mwenyezi Mungu atimize jambo lilio kuwa liwe. Na mambo yote hurejezwa kwa Mwenyezi Mungu.
 
45Enyi mlio amini! Mkikutana na jeshi, basi kueni imara, na mkumbukeni Mwenyezi Mungu sana ili mpate kufanikiwa.
 
46Na mt'iini Mwenyezi Mungu na Mtume wake, wala msizozane mkaingiwa woga, na zikapotea nguvu zenu. Na subirini. Hakika Mwenyezi Mungu yu pamoja na wanao subiri.
 
47Wala msiwe kama wale walio toka majumbani mwao kwa fakhari na kujionyesha kwa watu, na wakawazuilia watu Njia ya Mwenyezi Mungu. Na Mwenyezi Mungu ameyazunguka yote wanayo yafanya.
 
48Na pale Shet'ani alipo wapambia vitendo vyao, na akawaambia: Hapana watu wa kukushindeni hii leo, na hali mimi ni mlinzi wenu. Yalipo onana majeshi mawili, akarudi nyuma, na akasema: Mimi si pamoja nanyi. Mimi naona msiyo yaona. Mimi namwogopa Mwenyezi Mungu, na Mwenyezi Mungu ni mkali wa kuadhibu.
 
49Na walipo sema wanaafiki, na wale wenye ugonjwa nyoyoni mwao: Watu hawa dini yao imewadanganya. Na Mwenye kumtegemea Mwenyezi Mungu basi hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye nguvu Ametukuka, na Mwenye hikima.
 
50Na laiti ungeli ona Malaika wanapo wafisha wale walio kufuru wakiwapiga nyuso zao na migongo yao, na kuwaambia: Ionjeni adhabu ya Moto!
 
51Hayo ni kwa sababu ya yale yaliyo kwisha tangulizwa na mikono yenu, na hakika Mwenyezi Mungu si mwenye kuwadhulumu waja.
 
52Kama ada ya watu wa Firauni na walio kuwa kabla yao - walizikataa Ishara za Mwenyezi Mungu. Basi Mwenyezi Mungu aliwashika kwa sababu ya madhambi yao. Na hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye nguvu na mkali wa kuadhibu.
 
53Hayo ni kwa sababu Mwenyezi Mungu habadilishi kabisa neema alizo waneemesha watu, mpaka wao wabadilishe yaliyomo ndani ya nafsi zao. Na hakika Mwwnyezi Mungu ni Mwenye kusikia, Mwenye kujua.
 
54Ni kama ada ya watu wa Firauni na walio kabla yao - walizikanusha Ishara za Mola wao Mlezi, basi tukawateketeza kwa madhambi yao. Na tukawazamisha watu wa Firauni. Na wote walikuwa wenye kudhulumu.
 
55Hakika vinyama vilio viovu kabisa mbele ya Mwenyezi Mungu ni wale wanao kufuru, basi hao hawaamini;
 
56Wale ambao miongoni mwao umepatana nao ahadi, kisha wanavunja ahadi yao kila mara, wala hawamchi Mungu.
 
57Basi ukiwakuta vitani wakimbize walio nyuma yao ili wapate kukumbuka.
 
58Na ukichelea khiana kwa watu fulani basi watupilie ahadi yao kwa usawa. Hakika Mwenyezi Mungu hawapendi makhaini.
 
59Wala wasidhanie wale walio kufuru kwamba wao wametangulia mbele. La, wao hawatashinda.
 
60Basi waandalieni nguvu kama muwezavyo, na kwa farasi walio fungwa tayari-tayari, ili kuwatishia maadui wa Mwenyezi Mungu na maadui zenu, na wengineo ambao hamwajui, lakini Mwenyezi Mungu anawajua. Na mkitoa chochote katika Njia ya Mwenyezi Mungu mtarudishiwa, na wala nyinyi hamtadhulumiwa.
 
61Na wakielekea amani nawe pia elekea, na mtegemee Mwenyezi Mungu. Hakika Yeye ndiye Mwenye kusikia Mwenye kujua.
 
62Na wakitaka kukukhadaa basi Mwenyezi Mungu atakutosheleza. Kwani Yeye ndiye aliye kuunga mkono kwa nusura yake na kwa Waumini.
 
63Na akaziunga nyoyo zao. Na lau wewe ungeli toa vyote viliomo duniani usingeli weza kuziunga nyoyo zao, lakini Mwenyezi Mungu ndiye aliye waunganisha. Hakika Yeye ndiye Mtukufu Mwenye nguvu na Mwenye hikima.
 
64Ewe Nabii! Mwenyezi Mungu anakutoshelezea wewe na Waumini walio kufuata.
 
65Ewe Nabii! Wahimize Waumini wende vitani. Wakiwapo kati yenu ishirini wanao subiri watawashinda mia mbili. Na wakiwapo kati yenu mia watawashinda elfu moja katika walio kufuru. Kwa sababu wao ni watu wasio fahamu.
 
66Sasa Mwenyezi Mungu amekupunguzieni, na anajua kuwa upo udhaifu kwenu. Kwa hivyo wakiwa wapo watu mia moja kati yenu wenye kusubiri watawashinda mia mbili. Na wakiwapo elfu moja watawashinda elfu mbili, kwa idhini ya Mwenyezi Mungu. Na Mwenyezi Mungu yu pamoja na wenye kusubiri.
 
67Haimfalii Nabii yeyote kuwa na mateka mpaka awe ameshinda baraabara katika nchi. Mnataka vitu vya dunia, na Mwenyezi Mungu anataka Akhera. Na Mwenyezi Mungu ni Mtukufu Mwenye nguvu Mwenye hikima.
 
68Lau isingeli kuwa hukumu iliyo kwisha tangulia kutoka kwa Mwenyezi Mungu ingeli kupateni adhabu kubwa kwa vile mlivyo chukua.
 
69Basi kuleni katika mlivyo teka, ni halali na vizuri, na mcheni Mwenyezi Mungu. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusamehe na Mwenye kurehemu.
 
70Ewe Nabii! Waambie mateka waliomo mikononi mwenu: Kama Mwenyezi akiona kheri yoyote nyoyoni mwenu atakupeni bora kuliko vilivyo chukuliwa kwenu, na atakusameheni. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusamehe Mwenye kurehemu.
 
71Ikiwa wanataka kukufanyia khiana, wao walikwisha mfanyia khiana Mwenyezi Mungu kabla yake, na Yeye akakuwezesha kuwashinda. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kujua Mwenye hikima.
 
72Hakika wale walio amini na wakahama na wakapigania Njia ya Mwenyezi Mungu kwa mali yao na nafsi zao, na wale walio toa mahala pa kukaa, na wakanusuru, hao ni marafiki na walinzi wao kwa wao. Na wale walio amini lakini hawakuhama, nyinyi hamna waajibu wa ulinzi kwao hata kidogo mpaka wahame. Lakini wakiomba msaada kwenu katika Dini, basi ni juu yenu kuwasaidia, isipo kuwa juu ya watu ambao yapo mapatano baina yenu na wao. Na Mwenyezi Mungu anayaona mnayo yatenda.
 
73Na wale walio kufuru ni marafiki wenyewe kwa wenyewe. Msipo fanya hivi itakuwako fitna katika nchi na fisadi kubwa.
 
74Na walio amini wakahama na wakapigana Jihadi katika Njia ya Mwenyezi Mungu, na walio toa mahala pa kukaa na wakanusuru, hao ndio Waumini wa kweli. Watapata msamaha wa Mwenyezi Mungu na kuruzukiwa kwema.
 
75Na watakao amini baadaye na wakahajiri, na wakapigana Jihadi pamoja nanyi, basi hao ni katika nyinyi. Na jamaa wa nasaba wanastahikiana wenyewe kwa wenyewe zaidi katika Kitabu cha Mwenyezi Mungu. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye kujua kila kitu.